11 Basi Wayahudi wakamtafuta kwenye sikukuu, wakasema, Yuko wapi yule?
12 Kukawa na manung’uniko mengi katika makutano juu yake. Wengine wakasema, Ni mtu mwema. Na wengine wakasema, Sivyo; bali anawadanganya makutano.
13 Walakini hakuna mtu aliyemtaja waziwazi, kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi.
14 Hata ikawa katikati ya sikukuu Yesu alikwea kuingia hekaluni, akafundisha.
15 Wayahudi wakastaajabu wakisema, Amepataje huyu kujua elimu, ambaye hakusoma?
16 Basi Yesu akawajibu, akasema, Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.
17 Mtu akipenda kuyatenda mapenzi yake, atajua habari ya yale mafunzo, kwamba yatoka kwa Mungu, au kwamba mimi nanena kwa nafsi yangu tu.