Eze. 31:12-18 SUV

12 Na wageni, watu wa mataifa watishao, wamemkatilia mbali na kumwacha; juu ya milima na katika mabonde yote matawi yake yameanguka, na vitanzu vyake vimevunjika karibu na mifereji yote ya nchi; na watu wote wa dunia wameshuka, wakitoka katika uvuli wake na kumwacha.

13 Juu ya magofu yake ndege wote wa angani watakaa, na wanyama wote wa jangwani watakuwa juu ya matawi yake;

14 kusudi mti wo wote, ulio karibu na maji, usijitukuze kwa sababu ya kimo chake, wala usitie kilele chake kati ya mawingu, wala mashujaa wake wasisimame katika kimo chao kirefu, naam, wote wanywao maji; maana wote wametolewa wafe, waende pande za chini za nchi, kati ya wanadamu, pamoja nao washukao shimoni.

15 Bwana MUNGU asema hivi, Katika siku ile alipotelemka mpaka kuzimu naliamuru matanga, nalikifunika kilindi kwa ajili yake, nikiizuia mito yake, nayo maji makuu yalizuiwa; naliamuru Lebanoni kumwombolezea, na miti yote ya kondeni ilizimia kwa ajili yake.

16 Niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake, hapo nilipomtupa chini mpaka kuzimu, pamoja nao washukao shimoni; na miti yote ya Adeni, miti iliyo miteule na iliyo mizuri ya Lebanoni, yote inywayo maji, ilifarijika pande za chini za nchi.

17 Hao nao walitelemka kuzimuni pamoja naye kwa watu waliouawa kwa upanga; naam, wale waliokuwa mkono wake, waliokaa chini ya uvuli wake kati ya mataifa.

18 Umefanana na nani, hivi katika utukufu na ukuu, kati ya miti ya Adeni? Lakini utashushwa pamoja na miti ya Adeni, hata pande za chini za nchi; utalala kati ya hao wasiotahiriwa; pamoja na hao waliouawa kwa upanga. Huyu ndiye Farao, na jamii yote ya watu wake, asema Bwana MUNGU.