17 Basi, akawaacha, akatoka nje ya mji na kwenda Bethania, akalala huko.
18 Yesu alipokuwa anarudi mjini asubuhi na mapema, aliona njaa.
19 Akauona mtini mmoja kando ya njia, akauendea; lakini aliukuta hauna chochote ila majani matupu. Basi, akauambia, “Usizae tena matunda milele!” Papo hapo huo mtini ukanyauka.
20 Wanafunzi walipouona walishangaa wakisema, “Kwa nini mtini huu umenyauka ghafla?”
21 Yesu akawajibu, “Kweli nawaambieni, kama mkiwa na imani bila kuwa na mashaka, mnaweza si tu kufanya hivyo, bali hata mkiuambia mlima huu: ‘Ngoka ukajitose baharini,’ itafanyika hivyo.
22 Na mkiwa na imani, chochote mtakachoomba kwa sala, mtapata.”
23 Yesu aliingia hekaluni, akawa anafundisha. Alipokuwa akifundisha, makuhani wakuu na wazee wa watu wakamwuliza, “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Nani amekupa mamlaka haya?”