1 Ikawa Yesu alipokwisha kuwaagiza wanafunzi wake kumi na wawili, alitoka huko kwenda kufundisha na kuhubiri katika miji yao.
2 Naye Yohana aliposikia huko gerezani matendo yake Kristo, alituma wanafunzi wake, kumwuliza,
3 Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?
4 Yesu akajibu akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana mnayoyasikia na kuyaona;
5 vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.
6 Naye heri awaye yote asiyechukizwa nami.
7 Na hao walipokwenda zao, Yesu alianza kuwaambia makutano habari za Yohana, Mlitoka kwenda nyikani kutazama nini? Unyasi ukitikiswa na upepo?