62 Kisha Kuhani Mkuu akasimama akamwambia, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini?
63 Lakini, Yesu akanyamaza. Kuhani Mkuu akamwambia, Nakuapisha kwa Mungu aliye hai, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.
64 Yesu akamwambia, Wewe umesema; lakini nawaambieni, Tangu sasa mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa nguvu, akija juu ya mawingu ya mbinguni.
65 Ndipo Kuhani Mkuu akararua mavazi yake, akisema, Amekufuru; mna haja gani tena ya mashahidi? Tazameni, sasa mmesikia hiyo kufuru yake;
66 mwaonaje ninyi? Wakajibu, wakasema, Imempasa kuuawa.
67 Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi,
68 wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga?