7 Huko, mtakula mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, na mtafurahi nyinyi pamoja na watu wa nyumbani mwenu kwa ajili ya mafanikio yenu aliyowabarikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
8 “Msifanye kama tunavyofanya sasa, kila mtu kama apendavyo mwenyewe;
9 kwa sababu bado hamjaingia mahali pa kupumzikia na katika urithi anaowapeni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
10 Lakini mtakapovuka mto Yordani na kuishi katika nchi ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawapa mu irithi, na atakapowapatia pumziko msisumbuliwe na adui zenu wote watakaowazunguka ili muishi salama,
11 basi huko mahali Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atakapochagua ili jina lake likae, hapo ndipo mtakapopeleka kila kitu ninachowaamuru: Tambiko zenu za kuteketeza na sadaka zenu, zaka zenu na matoleo yenu, na sadaka zenu za nadhiri mnazoahidi kumtolea Mwenyezi-Mungu.
12 Huko mtafurahi mbele yake Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nyinyi pamoja na watoto wenu wa kiume na wa kike, watumishi wenu wa kiume na wa kike, na Walawi wanaoishi katika miji yenu, maana wao hawana sehemu wala urithi kati yenu.
13 Jihadharini msitoe sadaka zenu za kuteketezwa mahali popote mnapopaona;