24 Akalala Yehoramu na baba zake, akazikwa pamoja na baba zake mjini mwa Daudi; na Ahazia mwanawe akatawala mahali pake.
25 Katika mwaka wa kumi na mbili wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda alianza kutawala.
26 Ahazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu. Na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri mfalme wa Israeli.
27 Akaiendea njia ya nyumba ya Ahabu, akafanya yaliyo mabaya machoni pa BWANA, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu, kwa kuwa alikuwa mkwe wa jamaa ya Ahabu.
28 Akaenda pamoja na Yoramu mwana wa Ahabu ili kupigana na Hazaeli mfalme wa Shamu, huko Ramoth-gileadi; nao Washami wakamtia Yoramu jeraha.
29 Akarudi Yoramu mfalme, auguzwe katika Yezreeli jeraha walizotia Washami huko Rama alipopigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda akashuka amtazame Yoramu mwana wa Ahabu huko Yezreeli, kwa sababu alikuwa hawezi.