12 Basi Abneri akatuma wajumbe kwa Daudi mahali alipokuwapo, akisema, Nchi hii ni ya nani? Fanya agano nami, na tazama, mkono wangu utakuwa pamoja nawe, ili kuwaleta Israeli wote kwako.
13 Daudi akasema, Vema, nitafanya agano nawe, lakini nina sharti moja nitakalo kwako, nalo ni hili; Hutaniona uso wangu, isipokuwa uniletee Mikali, binti Sauli, hapo ujapo kuniona uso wangu.
14 Basi Daudi akatuma wajumbe kwa Ishboshethi, mwana wa Sauli, kusema, Nipe mke wangu Mikali, niliyemposa kwa govi mia za Wafilisti.
15 Basi Ishboshethi akatuma watu, akamnyang’anya Paltieli, mwana wa Laishi, mumewe, mwanamke huyo.
16 Huyo mumewe akafuatana naye, akiendelea na kulia, akamfuata mpaka Bahurimu. Ndipo Abneri akamwambia, Haya, rudi. Naye akarudi.
17 Basi Abneri akafanya mashauri na wazee wa Israeli, akasema, Zamani mlitaka Daudi awamiliki;
18 basi, sasa, fanyeni hayo; kwa maana BWANA amemtaja Daudi, akisema, kwa mkono wa mtumishi wangu, Daudi, nitawaokoa watu wangu Israeli katika mikono ya Wafilisti, na katika mikono ya adui zao wote.