4 Tena akawaamuru watu waliokaa Yerusalemu, watoe sehemu ya makuhani na Walawi, ili hao wajibidiishe katika torati ya BWANA.
5 Mara ilipotangaa amri, wana wa Israeli wakatoa kwa wingi malimbuko ya nafaka, na divai, na mafuta, na asali, na mazao yote ya mashamba; na zaka za vitu vyote wakazileta nyingi.
6 Nao wana wa Israeli na Yuda, waliokaa mijini mwa Yuda, wakaleta pia zaka za ng’ombe na kondoo, na zaka za vitu vilivyowekwa wakfu, alivyowekewa BWANA, Mungu wao, wakaviweka chungu chungu.
7 Katika mwezi wa tatu wakaanza kuweka misingi ya hizo chungu, wakazimaliza katika mwezi wa saba.
8 Hata walipokuja Hezekia na wakuu, na kuziona zile chungu, wakamhimidi BWANA, na watu wake Israeli.
9 Ndipo Hezekia akaulizana na makuhani na Walawi katika habari ya hizo chungu.
10 Azaria kuhani mkuu, wa nyumba ya Sadoki, akamjibu, akasema, Tangu watu walipoanza kuleta matoleo nyumbani kwa BWANA, tumekula na kushiba, na kusaza tele; kwa kuwa BWANA amewabariki watu wake; na kilichosalia ndiyo akiba hii kubwa.