Yer. 40:6-12 SUV

6 Basi, Yeremia akaenda kwa Gedalia, mwana wa Ahikamu, huko Mizpa, akakaa pamoja naye kati ya watu wale waliosalia katika nchi.

7 Kisha, wakuu wote wa majeshi waliokuwa katika bara, wao na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babeli amemweka Gedalia, mwana wa Ahikamu, kuwa liwali juu ya nchi, na kwamba amemkabidhi wanaume na wanawake na watoto, na baadhi ya maskini wa nchi wasiochukuliwa mateka Babeli;

8 ndipo wakamwendea Gedalia huko Mizpa; nao ni hawa, Ishmaeli, mwana wa Nethania, na Yohana na Yonathani, wana wa Karea, na Seraya, mwana wa Tanhumethi, na wana wa Efai, Mnetofa, na Yezania, mwana wa Mmaaka, wao na watu wao.

9 Na Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, akawaapia wao na watu wao, akisema, Msiogope kuwatumikia Wakaldayo; kaeni katika nchi, mkamtumikie mfalme wa Babeli; nayo itawafaa.

10 Na mimi, tazama, nitakaa Mizpa, ili nisimame mbele ya Wakaldayo watakaotujilia; lakini ninyi chumeni divai, na matunda ya wakati wa jua, na mafuta, mkaviweke vitu hivyo katika vyombo vyenu, mkakae katika miji yenu mliyoitwaa.

11 Kadhalika waliposikia Wayahudi wote, waliokuwa katika Moabu, na kati ya wana wa Amoni, na hao waliokuwa katika Edomu, na hao waliokuwa katika nchi zote, ya kuwa mfalme wa Babeli amewaachia Yuda mabaki, na ya kuwa amemweka Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, juu yao;

12 basi, Wayahudi wote wakarudi kutoka kila mahali walikofukuzwa wakaenda mpaka nchi ya Yuda, wakamwendea Gedalia huko Mizpa, wakakusanya divai, na matunda ya wakati wa jua mengi sana.