18 Na amiri wa askari walinzi akamtwaa Seraya, kuhani mkuu, na Sefania, kuhani wa pili, na wale walinzi watu wa mlango;
19 na katika mji akamtwaa towashi mmoja, aliyewasimamia watu wa vita; na watu watano katika wale waliosimama mbele ya mfalme, walioonekana mjini; na katibu wa jemadari wa jeshi, aliyewaandika watu wa nchi; na watu sitini katika watu wa nchi, walioonekana mjini.
20 Kisha Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawatwaa hao, akawaleta kwa mfalme wa Babeli huko Ribla.
21 Naye mfalme wa Babeli akawapiga, na kuwaua huko Ribla katika nchi ya Hamathi. Hivyo Yuda wakachukuliwa utumwani kutoka nchi yao.
22 Na kwa habari ya watu waliosalia katika nchi ya Yuda, aliowasaza Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akamweka Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani awe liwali juu yao.
23 Kisha, wakuu wote wa majeshi, wao na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babeli amemweka Gedalia kuwa liwali, wakamwendea Gedalia huko Mispa; nao ni hawa, Ishmaeli mwana wa Nethania, na Yohana mwana wa Karea, na Seraya mwana wa Tanhumethi Mnetofa, na Yezania mwana wa Mmaaka, wao na watu wao.
24 Na Gedalia akawaapia wao na watu wao, akawaambia, Msiogope kwa ajili ya watumishi wa Wakaldayo; kaeni katika nchi; mkamtumikie mfalme wa Babeli; itakuwa vyema kwenu.