12 Wakasema, Ni uongo; haya, tuambie. Akasema, Aliniambia haya na haya, akisema, BWANA asema hivi, Nimekutia mafuta, uwe mfalme juu ya Israeli.
13 Basi wakafanya haraka, kila mtu akalitwaa vazi lake, na kulitia chini yake juu ya madaraja, wakapiga baragumu wakasema, Yehu ni mfalme.
14 Hivyo Yehu, mwana wa Yehoshafati, mwana wa Nimshi, akafanya fitina juu ya Yoramu.Basi Yoramu alikuwa akiulinda Ramoth-Gileadi, yeye na Israeli wote, kwa sababu ya Hazaeli mfalme wa Shamu.
15 Lakini mfalme Yoramu mwenyewe alikuwa amerudi, apate kupona jeraha zake alizotiwa na Washami, alipokuwa akipigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Yehu akasema, Kama hii ndiyo nia yenu, basi, msimwache hata mtu mmoja atoke mjini, ili aende kupeleka habari Yezreeli.
16 Basi Yehu akapanda gari lake kwenda Yezreeli; kwa maana Yoramu alikuwa amelala huko; na Ahazia mfalme wa Yuda alikuwa ameshuka ili kumtazama Yoramu.
17 Basi mlinzi alikuwa anasimama juu ya mnara wa Yezreeli, akaliona lile kundi la watu wa Yehu, alipokuwa akija, akasema, Naona kundi la watu. Yoramu akasema, Haya! Mtwae mpanda farasi mmoja, ukampeleke aende kuwalaki, na kuwauliza, Je! Ni amani?
18 Basi mpanda farasi mmoja akatoka awalaki, akasema, Mfalme asema hivi, Je! Ni amani? Yehu akasema, Wewe una nini na amani? Geuka unifuate. Yule mlinzi akatoa habari, akasema, Yule mjumbe amewafikilia, lakini harudi tena.