40 Hili lilikuwa onyo kwa Waisraeli kwamba mtu yeyote ambaye si kuhani, yaani asiye wa ukoo wa Aroni asiende madhabahuni kumfukizia Mwenyezi-Mungu ubani. La sivyo ataangamizwa kama Kora na wafuasi wake. Haya yote yalitendeka kama Mwenyezi-Mungu alivyomwambia Eleazari kwa njia ya Mose.
41 Kesho yake, Waisraeli wote walimnungunikia Mose na Aroni wakisema, “Mmewaua watu wa Mwenyezi-Mungu.”
42 Walipokusanyika mbele ya Mose na Aroni ili kutoa malalamiko yao, waligeuka kuelekea hema la mkutano, wakaona kuwa wingu limeifunika hema na utukufu wa Mwenyezi-Mungu ulikuwa umetokea hapo.
43 Mose na Aroni walikwenda, wakasimama mbele ya hema la mkutano,
44 na Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,
45 “Jitenge na watu hawa, niwaangamize mara moja!”Lakini wao wakajitupa chini kifudifudi.
46 Mose akamwambia Aroni, “Chukua chetezo chako, kitie moto na kukiweka kando ya madhabahu, kisha ukitie ubani halafu uende nacho haraka kwa watu na kuwafanyia upatanisho. Fanya haraka! Ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu imekwisha wafikia na pigo limeanza kuwashambulia.”