1 Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa BWANA;Kama mifereji ya maji huugeuza po pote apendapo.
2 Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe;Bali BWANA huipima mioyo.
3 Kutenda haki na hukumuHumpendeza BWANA kuliko kutoa sadaka.
4 Macho yenye kiburi, na moyo wa kutakabari,Hata ukulima wa waovu, ni dhambi.
5 Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu;Bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji.
6 Kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongoNi moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti.
7 Jeuri ya wabaya itawaondolea mbali;Kwa sababu wamekataa kutenda hukumu.
8 Njia yake aliyelemewa na dhambi imepotoka sana;Bali mtu aliye safi, kazi yake ni sawasawa.
9 Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini,Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.
10 Nafsi ya mtu mbaya hutamani uovu;Jirani yake hapati fadhili machoni pake.
11 Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima;Na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa.
12 Mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya;Jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia.
13 Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini,Yeye naye atalia, lakini hatasikiwa.
14 Kipawa cha siri hutuliza hasira;Na rushwa bindoni humliza ghadhabu kali.
15 Ni furaha yao wenye haki kutenda hukumu;Lakini ni uharibifu kwao watendao maovu.
16 Mtu aikosaye njia ya busaraAtakaa katika mkutano wao waliokufa.
17 Mtu apendaye anasa atakuwa maskini;Apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri.
18 Mtu asiye haki ni fidia ya wenye haki;Naye afanyaye hila ni badala ya watu wa adili.
19 Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika;Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi.
20 Kuna hazina ya thamani na mafuta katika maskani ya mwenye hekima;Bali mwanadamu aliye mpumbavu huyameza.
21 Aandamaye haki na fadhili,Ataona uhai na haki na heshima.
22 Mwenye hekima huupandia mji wao wenye nguvu;Na kuziangusha nguvu za tumaini lao.
23 Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake,Atajilinda nafsi yake na taabu.
24 Mwenye kiburi na kutakabari, jina lake ni mbishi;Hutenda mambo katika majivuno ya kiburi chake.
25 Matakwa yake mtu mvivu humfisha,Kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi.
26 Kuna atamaniye kwa choyo mchana kutwa;Bali mwenye haki hutoa wala hanyimi.
27 Sadaka ya wasio haki ni chukizo;Si zaidi sana ailetapo mwenye nia mbaya!
28 Shahidi wa uongo atapotea;Bali mtu asikiaye atasema maneno yadumuyo.
29 Asiye haki huufanya uso wake kuwa mgumu;Bali mtu mnyofu huzifikiri njia zake.
30 Hapana hekima, wala ufahamu,Wala shauri, juu ya BWANA.