19 Naye Kora akawakusanya watu wote pamoja, wakasimama mbele ya Mose na Aroni ambao walikuwa mlangoni mwa hema la mkutano. Ndipo utukufu wa Mwenyezi-Mungu ukawatokea watu wote!
20 Hapo Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni,
21 “Jitengeni na watu hawa, niwaangamize sasa hivi.”
22 Lakini Mose na Aroni wakajitupa chini kifudifudi na kusema, “Ee Mwenyezi-Mungu uliye asili ya uhai wa binadamu wote. Je, mtu mmoja akikukosea, utaikasirikia jumuiya nzima?”
23 Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,
24 “Waambie watu waondoke karibu na makao ya hema ya Kora, Dathani na Abiramu.”
25 Basi, Mose akaenda kwa Dathani na Abiramu, akifuatwa na wazee wa Israeli.