14 Nami nitaishibisha roho ya makuhani kwa unono, na watu wangu watashiba kwa wema wangu, asema BWANA
15 BWANA asema hivi,Sauti imesikiwa Rama,kilio, na maombolezo mengi,Raheli akiwalilia watoto wake;asikubali kufarijiwa kwa watoto wake, kwa kuwa hawako,
16 BWANA asema hivi,Zuia sauti yako, usilie,na macho yako yasitoke machozi;Maana kazi yako itapata thawabu,nao watakuja tena toka nchi ya adui;Ndivyo asemavyo BWANA.
17 Tena liko tumaini kwa siku zako za mwisho, asema BWANA; na watoto wako watarejea hata mpaka wao wenyewe.
18 Hakika nimemsikia Efraimu, akijililia hivi, Umeniadhibu, nami nikaadhibika, kama ndama asiyeizoelea nira; unigeuze, nami nitageuzwa; kwa maana wewe u BWANA, Mungu wangu.
19 Hakika baada ya kugeuzwa kwangu, nalitubu; na baada ya kufundishwa kwangu, nalijipiga pajani; nalitahayarika, naam, nalifadhaika, kwa sababu naliichukua aibu ya ujana wangu.
20 Je! Efraimu siye mwanangu mpendwa? Je! Siye mtoto apendezaye? Maana kila nisemapo neno juu yake, ningali nikimkumbuka sana; kwa sababu hiyo moyo wangu unataabika kwa ajili yake; bila shaka nitamrehemu, asema BWANA.