32 Lakini nyinyi, mtafia humuhumu jangwani.
33 Watoto wenu watatangatanga na kutaabika humu jangwani kwa muda wa miaka arubaini kwa ajili ya ukosefu wenu wa imani mpaka mtu wenu wa mwisho atakapofia jangwani.
34 Kutokana na makosa yenu, mtataabika kwa muda wa miaka arubaini, sawa na zile siku arubaini mlizopeleleza ile nchi, mwaka mmoja kwa kila siku moja; mtatambua kwamba mimi nimechukizwa.
35 Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema: Hakika nitawatenda hivyo nyinyi nyote mliokusanyika hapa kunipinga. Wote wataishia humuhumu jangwani na ni humu watakamofia.”
36 Wale watu ambao Mose aliwatuma kwenda kuipeleleza ile nchi waliorudi na kusababisha watu wamnungunikie Mwenyezi-Mungu kwa kuleta taarifa mbaya dhidi ya nchi,
37 watu hao waliotoa taarifa ya uovu kuhusu hiyo nchi, walikufa kwa pigo mbele ya Mwenyezi-Mungu.
38 Lakini Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, walibaki hai miongoni mwa wale watu waliokwenda kuipeleleza nchi.