11 Kisha ndugu zake, dada zake na rafiki wote waliomfahamu hapo awali wakamwendea nyumbani kwake, wakala chakula pamoja naye. Wakampa pole na kumfariji kwa ajili ya mateso yote ambayo Mwenyezi-Mungu alikuwa amemletea. Kila mmoja wao akampa Yobu fedha na pete ya dhahabu.
12 Katika miaka ya Yobu iliyofuata Mwenyezi-Mungu alimbariki zaidi kuliko hata alivyokuwa amembariki pale awali. Basi Yobu akawa na kondoo 14,000, ngamia 6,000, ng'ombe 2,000 na punda majike 1,000.
13 Alikuwa pia na watoto wa kiume saba na wa kike watatu.
14 Binti yake wa kwanza alimpa jina Yemima, wa pili Kezia, na wa mwisho Keren-hapuki.
15 Katika nchi yote hiyo hapakuwa na wanawake waliokuwa wazuri kama mabinti wa Yobu. Baba yao akawaachia urithi kama alivyowaachia kaka zao.
16 Baada ya hapo, Yobu aliishi miaka 140, akawaona wajukuu na vitukuu vyake vyote hadi kizazi cha nne.
17 Basi, Yobu akafariki akiwa mzee wa miaka mingi.