Zaburi 34 BHN

Sifa kwa wema wa Mungu

(Zaburi ya Daudi alipojifanya mwendawazimu mbele ya Abimeleki)

1 Nitamtukuza Mwenyezi-Mungu nyakati zote,sitaacha kamwe kuzitamka sifa zake.

2 Mimi nitaona fahari juu ya Mwenyezi-Mungu,wanyonge wasikie na kufurahi.

3 Mtukuzeni Mwenyezi-Mungu pamoja nami,sote pamoja tulisifu jina lake.

4 Nilimwomba Mwenyezi-Mungu naye akanijibu,na kuniondoa katika hofu zangu zote.

5 Mgeukieni Mungu mpate kufurahi;nanyi hamtaaibishwa kamwe.

6 Maskini alimlilia Mwenyezi-Mungu, naye akamsikia,na kumwokoa katika taabu zake zote.

7 Malaika wa Mwenyezi-Mungu huwalinda wote wamchao,na kuwaokoa katika hatari.

8 Jaribuni mwone Mwenyezi-Mungu alivyo mwema.Heri mtu anayekimbilia usalama kwake.

9 Mcheni Mwenyezi-Mungu enyi watakatifu wake;maana wenye kumcha hawatindikiwi na kitu.

10 Hata wanasimba hutindikiwa na kuona njaa;lakini wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu hawakosi chochote chema.

11 Njoni enyi vijana mkanisikilize,nami nitawafundisha kumcha Mwenyezi-Mungu.

12 Je, watamani kufurahia maisha,kuishi maisha marefu na kufurahia mema?

13 Basi, acha kusema mabaya,na kuepa kusema uongo.

14 Jiepushe na uovu, utende mema;utafute amani na kuizingatia.

15 Mwenyezi-Mungu huwaangalia waadilifu,na kusikiliza malalamiko yao;

16 lakini huwapinga watu watendao maovu,awafutilie mbali kutoka duniani.

17 Waadilifu wakimlilia Mwenyezi-Mungu yeye huwasikia,na kuwaokoa katika taabu zao zote.

18 Mwenyezi-Mungu yu karibu na waliokufa moyo;huwaokoa wote waliokata tamaa kabisa.

19 Mateso ya mwadilifu ni mengi,lakini Mwenyezi-Mungu humwokoa kutoka yote.

20 Huvilinda viungo vya mwili wake wote,hakuna hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.

21 Ubaya huwaletea waovu kifo;wanaowachukia waadilifu wataadhibiwa.

22 Mwenyezi-Mungu huokoa maisha ya watumishi wake,wote wanaomkimbilia hawataadhibiwa.