Zaburi 22 BHN

Kilio

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa utenzi wa kulungu wa alfajiri. Zaburi ya Daudi)

1 Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?Mbona uko mbali sana kunisaidia,mbali na maneno ya kilio changu?

2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu;napiga yowe usiku, lakini nafuu sipati.

3 Hata hivyo, wewe ni mtakatifu;wewe watawala na kusifiwa na Waisraeli.

4 Wazee wetu walikutegemea;walikutegemea, nawe ukawaokoa.

5 Walikulilia wewe, wakaokolewa;walikutegemea, nao hawakuaibika.

6 Lakini mimi ni mdudu tu, wala si mtu;nimepuuzwa na kudharauliwa na watu.

7 Wote wanionao hunidhihaki;hunifyonya na kutikisa vichwa vyao.

8 Husema: “Alimtegemea Mwenyezi-Mungu,basi, Mungu na amkomboe!Kama Mungu anapendezwa naye,basi, na amwokoe!”

9 Lakini ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu,uliniweka salama kifuani pa mama yangu.

10 Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu.Tangu nilipozaliwa wewe umekuwa Mungu wangu.

11 Usikae mbali nami, kwani taabu imekaribia;wala hakuna wa kunisaidia.

12 Maadui wengi wanizunguka kama fahali;wamenisonga kama fahali wakali wa Bashani!

13 Wanafunua vinywa vyao kama simba,tayari kushambulia na kurarua.

14 Nimekwisha kama maji yaliyomwagika;mifupa yangu yote imeteguka;moyo wangu ni kama nta,unayeyuka ndani mwangu.

15 Koo langu limekauka kama kigae;ulimi wangu wanata kinywani mwangu.Umeniacha kwenye mavumbi ya kifo.

16 Genge la waovu limenizunguka;wananizingira kama kundi la mbwa;wamenitoboa mikono na miguu.

17 Nimebaki mifupa mitupu;maadui zangu waniangalia na kunisimanga.

18 Wanagawana nguo zangu,na kulipigia kura vazi langu.

19 Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu, usikae mbali nami;ewe msaada wangu, uje haraka kunisaidia.

20 Iokoe nafsi yangu mbali na upanga,yaokoe maisha yangu makuchani mwa mbwa hao!

21 Uniokoe kinywani mwa simba;iokoe nafsi yangu dhaifu toka pembe za nyati hao.

Wimbo wa shukrani

22 Nitawasimulia ndugu zangu matendo yako;nitakusifu kati ya kusanyiko lao:

23 Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, msifuni!Mtukuzeni enyi wazawa wote wa Yakobo!Mcheni Mungu enyi wazawa wote wa Israeli!

24 Maana yeye hapuuzi au kudharau unyonge wa mnyonge;wala hajifichi mbali naye,ila humsikia anapomwomba msaada.

25 Kwa sababu yako ninakusifukatika kusanyiko kubwa la watu;nitatimiza ahadi zangu mbele yao wakuchao.

26 Maskini watakula na kushiba;wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu watamsifu.Mungu awajalie kuishi milele!

27 Ulimwengu wote utakumbuka na kumrudia Mwenyezi-Mungu;jamaa zote za mataifa zitamwabudu.

28 Maana Mwenyezi-Mungu ni mfalme;yeye anayatawala mataifa.

29 Wenye kiburi wote duniani watasujudu mbele yake;wote ambao hufa watainama mbele yake,wote ambao hawawezi kudumisha uhai wao.

30 Vizazi vijavyo vitamtumikia;watu watavisimulia habari za Mwenyezi-Mungu,

31 watatangaza matendo yake ya wokovu.Watu wasiozaliwa bado wataambiwa:“Mwenyezi-Mungu ndiye aliyefanya hayo!”